Jumanne, 5 Julai 2016



BATUL AFFAR ISMAIL NA WENZAKE
CHAWAKAMA-SUZA
MAKALA
KUHUSU KUIMARIKA NA KUFA KWA JANDO, UNYANGO NA MICHEZO YA WATOTO ZANZIBAR KAMA NI SANAA YA MAONYESHO
1.0  Utangulizi
      Asili ya jando na unyago
      Maana ya Sanaa za maonyesho
      Maana ya Jando na Unyago
       Sababu za kuitwa Jando na Unyago
      Lengo la Unyago na  Jando
      kuimarika na kufa  kwa jando na unyago.
      Maana ya michezo ya watoto
       Mafunzo ya michezo ya watoto
      Kuimarika na kufa kwa michezo ya watoto
       Dosari
       Mapendekezo
2.0 Asili ya jando na unyago
Kwa mujibu wa bwana Mvita Kassim mwanajamii wa mjini Zanzibar ambaye tulifanya nae mahojiano ya ana kwa ana alisema kwamba  jando Zanzibar linatokana na mila na desturi za uislamu ambazo zinamtaka  muislamu  apate sunna na lazima afate utaratibu huo. Asili ya jando ni nchini Lamu limekuja kutokana na maingiliano ya watu kutoka Lamu kuja Zanzibar kwa shughuli za kibiashara na misafara ya kidini. Watoto walikuwa wanafanyiwa jando wakiwa na umri wa miaka 8– 15 hapo hupewa mafunzo maalum ambayo huzingatia anachoelezwa. Na shughuli ya kutahiriwa hufanywa alfajiri kando ya mji na hualikwa mangariba wa kila upande kuhudhuriya shughuli ya jando ili kuepusha mambo ya kishirikina ambayo hufanyika wakati wa kutahiriwa. Pia huwekwa migomba kwa ajili ya kukabidhiwa wale wazee ambao kwa bahati mbaya watoto wao walifariki katika zowezi la tohara.
Wari wakimaliza kutahiriwa hupakwa “Iodine” aidini na hupewa maji ya madafu wanywe ili wapate kukojowa sana na kidonda kipowe haraka. Pia bwana Mvita alisema katika mwambao wa pwani zikimalizika shughuli za jando na unyago hakuna mawasiliano kati ya mangariba na manyakanga kwa kuwakutanisha wari wa kike na wakiume kwa ajili ya kufanya kwa  vitendo yale mafunzo waliyofundishwa unyagoni au jandoni. Aidha alisema kwamba kuna tofauti kubwa ya vijana waliopata mafunzo ya jando na wasiopata mafunzo ya jando. Waliopata mafunzo huwa wanakatazwa kufanya tendo la ndowa kabla ya kuowa pia kijana akitahiriwa mdogo sana kama miezi miwili au siku arubaini anapofika miaka 20 nguvu za kiume zinapungua tofauti na alietahiriwa akiwa na umri wa miaka 8 au 15 au zaidi ya hapo.



 2.0.1 Sababu za kuitwa jando
Ni hiyo silabi ya mwanzo isemayo ja kwa maana ya ukubwa. Na kutowa methali isemayo “ukubwa ni  jaa”.  Ja  hiyo imeshabihiana na jando kimaana.
Na kwa mujibu wa bwana Rashid na Bi Fatma wa mjini Fuoni wanasema kwamba katika miaka ya 60 vijana walifanyiwa tohara kati ya miaka 14 -20 miaka hii walikuwa wakipewa mafunzo ya ndowa. Katika miaka ya 70 watoto wa kiume walifanyiwa tohara wakiwa na umri wa miaka     12 – 16 hapa walifanyiwa sherehe na kupewa mafunzo ya ukakamavu. Katika miaka ya 80 watoto wa kiume walifanyiwa tohara wakiwa namiaka 5 -12 walifanyiwa sherehe tu. Na kuanzia miaka ya 90 mpaka kuendelea walifanyiwa tohara kuanzia siku 21 au miezi mitatu au mwaka mmoja ama miwili katika sehemu nyingi za mji wa Zanzibar.  
2.1 Lengo kuu la vijana kufanyiwa tohara
·         Lengo kuu lakufanyiwa tohara watoto wakiwa na umri mkubwa wenyewe wanasema kwamba ni kuoneshwa machungu ya kuona  kuwa uume si kitu cha masihara ukautia kwa mwanamke yeyote tu bali asubirie wakati muafaka wa ndowa yake  hali hii ilipelekea kupungua kwa  ngono uzembe.
·         Kumtayarisha kijana kushiriki katika mambo ya kuongoza jamii yake hususan hiyo ambayo atakwenda kuanza nayo maisha ya uwili.
2.2. 0  Asili  ya unyago Zanzibar
Kwa mujibu wa bwana Kassim unyago  Zanzibar asili yake  kutoka kwa Wangindo wanaoishi kusini mwa Tanzania na Wamanyema kutoka  Kigoma .Waarabu wa Zanzibar walipendezwa na mila hizo wakawa na ukaribu sana na watu wa jamii hizo mpaka kupelekea kuowa katika jamii za Wangindo na Wamanyema ili kufaidika na hayo mafunzo ya jadi.
2.2.1 Sababu ya kuitwa unyago
Ni manyago yanayofanyika kipindi cha wari kuwekwa ndani na wameita unyago kwasababu ndani ya unyago kuna vitisho, vitimbwi na mambo ya kinyama ambayo wanafanyiwa wari hao huwezi kuvielezea vyote ni siri ambazo hazitakiwi kutolewa nje. Mfano mwari anapelekwa ndani ya chumba chenye giza akisha lizoweya hilo giza anakuja mtu na koroboi anamwambia aangalie chumba kina nini mwari anakutana na mtu alielazwa chali kwenye kitanda cha kamba kapakwa rangi usoni na mwilini kisha katiwa na donge gumu la ladu mdomoni anaambiwa mtu yule amekufa fanya mizungu yako afufuke kisha anaachwa peke yake.
Pia hunyolewa nywele za siri kwa kupakwa jivu na kuvutwa nywele hizo kwa mkufu hawatumii kiwembe. Vilevile hulazwa mwanamke chali na kuambiwa wampandie juu na wakate viuno mpaka vikatike sawasawa. Hupewa mtu amsugue kwa pumba za mahindi au unga wakarafuu kama ni somo la kumsuguwa bwana huko aendako. Mambo yote anayofundishwa huko huambiwa ndio mambo atakayokutana nayo lakini hapo hupewa somo la usugu wa shida, vitisho, vituko na vitimbwi atakavyovipata kwa mumewe. Anasulubiwa kusudi apate kuizoweya hali hiyo ya mateso na anatakiwa astahamili sana .
Kwa mujibu wa Bi Fatma Juma wa mjini Zanzibar anasema sehemu mashuhuri za kufanyika jando na unyago ni mwembetanga, kisimamajongoo, kikwajuni na kwahani na kwa upande wa Pemba ambapo bado shughuli hizi zinafanyika ni kojani, micheweni na msuka. Na watu mashuhuri waliokuwa wakitajika kwa kufanya shughuli za unyago ni Bi fatma binti Baraka na Bi Kiboga kwa Zanzibar. Pia alifafanuwa kuwa mwanachama wa unyago kama anataka mtoto wake afanyiwe unyago anawaalika manyakanga wote lakini ndani yake anakuwepo nyakanga mkuu wa shughuli hiyo na nyakanga mkuu ndio anaetowa taarifa za kufanyika kwa unyago. Pia Bi Fatma alisema wakati wa kufanywa unyago ni magharibi na kama ni wari ambao hawakufikia muda wa kuolewa hukaa ndani kwa siku saba za ada ambazo mwari huvunja ungo. Siku ya saba mwari akipelekwa kwao hupambwa kwa kuvishwa nguo mpya na kusukwa minyosho. Na kama mwari kafikia umri wa kuolewa huwekwa ndani wiki mbili au miezi mitatu. Mwari  huvishwa kaniki sehemu ndogo tu ya kusitiri uchi wake.  Mwari huimbiwa nyimbo kama hii
“ Nifungulie  mlango nipite wee
Nifungulile wee nipite mimi”
Mwari huenda kufungua mlango kwa magoti na anatakiwa azungumze kwa ishara tu. Nyakanga humkabidhi mwari kikombe cha liwa ndio salamu yenyewe. Vilevile hakuna mawasiliano baina ya nyakanga na wari nyakanga kazi yake kutowa mafunzo tu na si kitu chengine. Inakuwepo na ngoma ya unyago ambayo manyakanga wasaidizi kazi yao kutoa nyimbo za mafunzo tu.    Mfano wa nyimbo ya unyago anayoimbiwa mwari.
“kanipe kanipe
Ulipokiweka kanipe
Kijaluba cha mwari kanipe
Tena pelekapeka kwa wakubwa wakarore”
Katika nyimbo hii mwari huambiwa akachukuwe ushanga uliowekwa kwenye kibao, ushanga huo huwa umezongwa kama jongoo aliyejikunja. Mwari huamrishwa akauchukue ushanga huo na aunyanyuwe kwa matako yake kisha akawakabidhi manyakanga wakuu.  Na akishindwa kuunyanyua ushanga kwa matako huimbiwa wimbo huu
“ Msungo kungwi we msungo
Mwari msungo we mwari
Kungwi alomtia mwari kitororo
Mwari wa nyakanga kitororo”
Kwa kumaanisha kungwi na mwari wake wote wasungo. Ili asalimike kungwi inampasa akauchukuwe yeye kwa matako aupeleke kwa nyakanga la sivyo mwari atapigwa shanga za kiuno mpaka kungwi aufikishe na mwari anaona ushanga unavyonyanyuliwa kwa matako.
2.3 Lengo la unyago kwa vijana wa kike.
·         Kujenga moyo wa ujasiri kwa kufuata yale yote anayoelekezwa kwa kutii amri.
·         Kupata heshima ya kuzungumza na mkubwa wake na atakapokuwa kwa mumewe.
·         Kutokujibizana na mkubwa wako
·         Kuwa mstahamilivu pindipo akipata mume mwenye mateso.
·         Kufundishwa usugu wa kupambana na matatizo atakayokumbana nayo.
2.4.0 Maana ya sanaa za maonyesho
kwa mujibu wa Semzaba (1997) anasema kwamba ni uonyeshaji wa maisha kisanaa ambapo mwonyeshaji na hadhiraa huwepo mahali pamoja na wakati mmoja.
Pia sanaa za maonyesho ni kitendo chochote chenye sifa nne za mchezo, mchezaji, uwanja wa kuchezea na watazamaji kama vile jando, unyago, kusalia mizimu na masimulizi ya hadithi. (Balisidya na  Muhando)
2.4.1  Maana ya Jando na unyago
kwa mujibu wa Muhando na Balisidya (1976) ni  aina mojawapo ya kiada yaani miviga ambayo hufanyika kwa wakati wake maalum ili kuadhimisha wari wanapobaleghe. Kwa ufupi ni ibada ya mpito kwa kuwa inasaidia watoto kupitia katika mabadiliko ya hadhi kiishara kutoka kuwa mtoto ambaye alikuwa akiishi katika vitendo vilivyokiuka taratibu za heshima na kuwa mtu ambaye sasa anapaswa kuishi katika mazingira ya taratibu za tabiya ya utulivu kwa  jamii na kuzifuata.
Kwahiyo unyago ni mfumo wa elimu isiyo rasmi inayotolewa na makungwi au nyakanga na ngariba kwa vijana ambao wanatoka katika umri wa utoto na kuingia katika utu uzima. Hapa hupata mafunzo yanayohusu stadi za maisha na jinsi ya kuishi na wenza wao.
Na jando ni kipindi cha mageuzi au mabadiliko ya mtoto kuwa mtu mzima ambaye anaweza kushiriki katika maongozi ya jamii yake. Jando hili linahusu watoto wa kiume wasiopungua umri wa miaka 15.
2.4.2 Msimu wa unyago na jando
Unyago na jando hufanyika wakati wa msimu wa mavuno na vyakula wanavyokula ni vya kawaida ambavyo huwa wanakula kila siku majumbani kwao pamoja na  vinywaji kama pombe ya mtama na togwa. Nyimbo huwa ni michepuko na kusherehesha shughuli ya unyago na jando. Walioko nje wasisikie kinachosemwa ndani wala kusikia sauti za wari.
2.4.3. Masharti ya unyago  
Masharti ya unyagoni kwamba kilichofanyika ndani hakiruhusiwi kutoka nje. Na ni mwiko kumhadithia mtu kilichofanyika ndani ya unyago au mambo uliyoelezwa ulipokuwa unyagoni.


2.4.4. Mazingira ya unyago na jando
Jando na unyago hufanyika porini au sehemu iliyo nje ya mji.
2.5 kuimarika kwa jando na unyago
Kwa mujibu wa Mvungi (1976) ametaja mambo matatu ambayo hufanyika katika jando nayo ni
·         Kumtahiri kijana kusimamia uishara wa kifo cha utoto wake.
      Mafunzo juu ya vipengele vya elimu ya utu uzima katika jamii yake kwa ujumla.
      Kutoka nje baada ya kumaliza mafunzo hupelekwa kuoga na kuvishwa nguo mpya.
kutokana na maelezo ya Mvungi na Omar jando na unyago yaliimarika kwasababu wazee walikuwa wanathamini mambo ya mila na utamaduni pia waliamini kuwa watoto wanapopata mafunzo ya jando na unyago wanakuwa wamekomaa kiakili na kimwili na kuweza kushiriki katika kuongoza familiya kwa kutowa ushauri na kufanya mambo mengine yanayohusu familiya.
kwahiyo unyago na jando yaliimarika kwasababu ya mashirikiano yaliopo baina ya jamii moja na nyengine. Pia mahitaji ya jamii hayakuwa makubwa sana kwa wakati ule na walizingatia zaidi mambo ya mila na desturi zake ambayo kwasasa ni mambo yaliyopita na hayawezi kurudi tena.
2.6 mafunzo ya jando
Omar na Mvungi (1981) wametaja baadhi ya mafunzo hayo kuwa ni -:
      kufunzwa adabu                                                                                                                        
      kujuwa umuhimu wa kazi
       kuyajuwa maisha ya utu uzima
       kuishi vyema
       kumtayarisha kijana kushiriki katika mambo ya kuongoza jamii
      kupata mafunzo ya mwili na akili.
2.7  Kufa kwa Jando na Unyago.
Kufa kwa unyago na jando ni kwasababu ya haya mambo ya wigo ambayo jamii yameiga kutoka nchi za magharibi ili kuchukuwa nafasi ya jando na unyago. Mfano singo, kitchen party nk mambo haya yamezuka ili kufupisha muda wa shughuli za unyago na jando.Gharama zinatumika ili kuoneshana makarama nani amefanya jambo jipya katika shughuli yake. Pia sababu nyengine ni kwamba shughuli hizi za jando na unyago hazikurithishwa kwa vizazi vipya kutokana  na kuonekana ni mila za kishezi zilizopitwa na wakati.
      MAANA
      Michezo ya watoto
      Mafunzo ya michezo ya watoto
      Kuimarika na kufa kwa michezo ya watoto.
3.0 Maana ya michezo ya watoto
Michezo ya watoto kwa mujibu wa Haji (2006) ni michezo ambayo watoto wanacheza katika mazingira yao wanayoishi. Watoto hufanya hivyo kutokana na kuiga mambo ambayo wanayoyaona katika jamii wanayoishi.
Michezo ya watoto iko mingi sana kama michezo ya kuigiza ya watoto, foliti, kuruka kamba, dama, kifichoficho, karata, vitendawili, chemshabongo, michezo inayoambatana na nyimbo kama kinyuli, kachiri, matango manemane nk. Wanapocheza michezo hii huwasaidia kuimarisha viungo vya mwili kwa kukimbia, hupata burudani kwa kuimba na kucheza pamoja na kuigiza michezo mbalimbali kama baba na mama, daktari, askari, pia kupanuwa akili zao katika kujipatia maarifa ya chemsha bongo na vitendawili.
3.1 kuimarika kwa michezo ya watoto
Michezo ya watoto iliwafanya kujenga urafiki kwa kukuza uhusiano uliopo baina ya mtoto na mtoto kutokana na malezi ya pamoja waliokuwa nayo majirani.  Pia michezo hiyo iliwapa nafasi watoto wawe huru katika kujifunza mambo mbalimbali, kupitia michezo yao hujifunza kuogelea, kuruka kamba, kuimba, kufanya mazoezi ya kukimbia, kucheza mpira nk. Vilevile ilijenga mashirikiano katika kuongozana cha kufanya ndani ya michezo yao kama kuwa daktari na kuigiza sehemu ya daktari na mgonjwa au kuigiza sehemu ya baba na mama kwa kuigiza matendo wanayoyaona majumbani kwao ama kuigiza nafasi ya mwalimu na mwanafunzi.                                                                                                  Pia kupitia michezo yao huwa wabunifu kila siku zikiendelea hubuni michezo mbalimbali kama  mchezo wa bui, mchezo wa farasi, nage, mdako, bao, hadifundo, ukuti, kinyuki kipenyapenya, kigurucheche ambayo huambatana na nyimbo zake.  Aidha kupitia michezo yao watoto huunda mbinu mbalimbali za kuweza kuwasiliana wakati ukifika wa kucheza michezo yao. Huanza kwa kuimba au kupiga miluzi ama kuitana majina wanayopeana katika michezo yao                                                                                        Kwahiyo hizo ndio sababu kuu zilizofanya michezo ya watoto iimarike kutokana na mambo ambayo watoto walikuwa wakiyafanya na kufaidika nayo wanapocheza.
3. 2 Mafunzo ya michezo ya watoto
      Watoto hupanuwa akili kwa kupata maarifa mapya kupitia michezo yao.
      Huwa wabunifu kwa kuigiza maigizo mbalimbali
      Kwa wale watoto wenye uzito katika kusema hupata mazoezi ya kujifunza kusema kwa haraka
      Huwaondolea aibu katika kusema mbele ya wenziwao na kuwafanya wawe wachangamfu.
3. 3 .0  Kufa kwa Michezo ya watoto
Michezo ya watoto imekufa kutokana na mabadiliko mbalimbali katika jamii ambayo yamesababishwa na muingiliano wa tamaduni tafauti katika jamii mbalimbali.                     mfano elimu, dini, ubakaji na uibiwaji wa watoto pamoja na maendeleo ya sayansi na teknolojia.
 3.3.1 Elimu
Iimechangia kwa kiasi kikubwa kufa kwa michezo ya watoto kwasababu  wanapokuwa maskuli watoto hupata nafasi ya kucheza ile michezo wanayocheza majumbani kwao pia masomo ya ziada kwa watoto hasa somo la kiengereza, hesabati na sayansi yamewafanya watoto wasiwe na nafasi ya kucheza kutokana na kuwa ule muda ambao wao walitakiwa wacheze wao huwa wanapata masomo ya ziada kwa ajili ya kuongeza maarifa zaidi.
3.3.2 Dini
Mafunzo wanayopata watoto wanapokuwepo katika madrasa zao. Mara nyingi watoto huwa wanafundishwa michezo ya kusali na kuepukana na ibilisi kwa kucheza michezo isiyo na maana. Hutumia muda wao wakucheza kwa kujifunza maulidi, kuhifadhi qur-ani, kusoma kasida, kusimuliwa visa vya mitume na kufundishwa michezo yenye maadili mema kwa jamii yao na kuandaliwa kuwa vijana wema.
3.3.3 Ubakaji na uibiwaji wa watoto
 Wimbi hili limepelekea kufa kwa michezo ya watoto kwasababu hakuna mzazi anayetaka mtoto wake akumbwe na kadhiya hiyo. Kwahiyo kila mzazi anafanya jitihada ili mwanawe asiwe mbali na nyumbani  kwao kwa kupoteza muda kucheza ovyo majumbani kwa watu. Mzee hufanya jitihada za kumnunulia vitabu mwanawe ajisomee nyumbani au aangalie michezo ya watoto kupitia televisheni au dvd ama aende twisheni kwa kuongeza maarifa.
3.3.4 Sayansi na teknolojia
Iimeuwa kabisa michezo ya watoto kwasababu watoto husikiliza vipindi vya hadithi na nyimbo kupitia redio, hushiriki katika kujibu masuali ya hadithi au kuimba nyimbo kupitia  vipindi vya hewani vya papo kwa papo. Hupata nafasi ya kushiriki vipindi mbalimbali vya televisheni na redio. Huangalia michezo ya kuigiza ya watoto wenzao katika stesheni nyengine za televisheni. Hucheza gemu kupitia kompyuta na kuangalia katuni mbalimbali kupitia dvd au video, viwanja vya pembea za kufurahishia watoto, vituo bubu vya kuchezea gemu mbalimbali kwa wale ambao hawana vitu hivyo majumbani mwao pamoja na sehemu za kuangalia wanyama kama Zala park na Zanzibar park. Maendeleo haya yamewafanya watoto wasiwe na muda wa kukaa pamoja na watoto wenzao kucheza kama zamani.
4.0 Dosari
·         Dosari nyingi zinazojitokeza katika jamii mbalimbali ni  kutokuelewa umuhimu wa utamaduni wa jamii inayohusika
·         .Wazee kutokuwarithisha watoto wao mambo ya kimila au watoto kuyapuuza kuona ni mila zilizopitwa na wakati  na kudhani kuwa ni mila za kishenzi. Kufa kwa unyago na jando ni wigo wa kuzuka mambo mapya katika jamii yaliopelekea kupuuzwa kwa mila hizo.
·         Kukosekana malezi ya pamoja kila mzazi analea wanawe apendavyo mwenyewe.
·         Kupungua kwa mashirikiano baina ya jirani na jirani.
·         Michezo ya watoto imekufa kutokana na maendeleo mbalimbali yaliyozuka katika jamii zetu na kupelekea kufa kabisa kwa michezo hiyo ingawa imekuja kwa njia ya video, redio na televisheni pamoja na viwanja vya kufurahishia watoto. Lakini imeondosha ule ukaribu waliokuwa nao watoto hapo zamani ukilinganisha na sasa.
·         Kukosekana kwa uaminifu miongoni mwa vijana, watoto na wazee inayopelekea watoto kubakwa ama kuibiwa.


5.0  Mapendekezo
Tumeona sababu mbalimbali zilizofanya kuimarika kwa jando na unyago pamoja na michezo ya watoto ni malezi bora na mashirikiano ya jamii moja kwenda nyengine. Pamoja na mafunzo na mbinu mbalimbali wazipatazo kupitia shughuli za kimila za jando na unyago na michezo ya watoto kama sanaa za maonyesho Zanzibar.
·         Ni mapendekezo kupitia makala hii kuwatafuta wazee mabalimbali wanaojuwa mambo ya unyago na jando na kuwaelimisha watu umuhimu wake kupitia magazeti, redio pamoja na televisheni
·         Kuanzisha vipindi mbalimbali kuhusu mambo ya mila, silka na tamaduni zetu kupitia    makongamano.
·         Kuanzishwa somo la utamaduni wetu kuanzia ngazi za msingi na sekondari
·         .Kutengenezwa vipindi maalum vinavyowahusu watoto ili wapate kuona watoto wa zamani walikuwa wanacheza michezo ipi.
·         Watoto kuelimishwa mafunzo na faida wanazozipata  kupitia michezo yao. Miongoni mwa mafunzo hayo ni stadi za maisha wanazofunzwa katika michezo yao ya kuigiza ama hadithi za paukwa pakawa.


MAREJEO
Haji, M. O. (2006). Vipera vya Fasihi Simulizi. Kidato cha 1- 4. Tanzania.
Makame F.. K. ( mahojiano ya ana kwa ana, 3 Aprili 2015)
 Mhando, P na Balisidya (1976). Fasihi na Sanaa Za Maonyesho. Tanzania Publishing                                                    House:  Dar-es-salaam.
  Muhammed, O.S. (2010).Tasnifu; Mchango Wa Nyimbo Za Unyago Katika Kumkomaza                                                         Mwari Kinyumba.
Mvungi, T. A. (1976). Fasihi Simulizi; Katika Sekondari. Taasisi Ya Elimu: Dar-es-salaam.
Rashid A. R. ( mahojiano ya ana kwa ana, 1 Aprili 2015)
 Semsaba, E. (1997). Tamthiliya ya Kiswahili. Chuo Kikuu Huriya Cha Tanzania:                                                          Dar-es-salaam.
 Taratibu  M. K.( Mahojiano ya ana kwa ana,  tarehe 20 Machi 2015).
     
.

Maoni 1 :

  1. Kwanza napenda kutoa pongezi kwa waandaji was makala hii, mada nzuri. Lakini hats hivyo, ninapenda kuuliza suala dogo;
    Jee, walengwa(wasomaji) was makala hii no waswahili pekeyao ndio uliwakusudia?
    Kama c hivyo? Back napenda kutoa ushauri kwamba in vyema ukaainisha maana ya baadhi ya misamiati iliyotumika katika makala hii, kwa mfano; kungwi, nyakanga, mwari, dingo. nk. Hii itasaidia kwa wale wageni wanaojifunza kiswahili na utaduni wa waswahili, kuelewa kwa urahisi makala hii watakapo tembelea blog hii, kwani misamiati hii kwao wao c famial.

    JibuFuta