Jumatatu, 4 Julai 2016



NAFASI YA JINSIA KATIKA HADITHI FUPIFUPI ZA KISWAHILI
Na Bishara Mohamed Ali 
CHAWAKAMA-SUZA
Jinsia ni mahusiano ya kijamii na kiutamaduni yanayozingatia mgawanyo wa majukumu kwa kuangalia jinsia ya kike au ya kiume.
Hadithi fupifupi ni aina ya kazi ya sanaa ya utanzu wa hadithi inayotumia lugha iliyoandikwa katika nathari au iliyo katika masimulizi kama haijaandikwa. (Msokile, 1992:199). Katika hadithi fupifupi za Kiswahili zimeoneshwa jinsia zote ambazo ni jinsia ya kike na jinsia ya kiume pamoja na dhima zao mbalimbali. Nitatumia hadithi fupi ya HAMNAZO, JIRANI MWAMINIFU, ULIMI WA DA MSIMU na MTU NA HAKI YAKE ili kutathmini nafasi ya jinsia ilivyooneshwa katika hadithi hizo.
Kwa kuanzia na hadithi ya Hamnazo nafasi ya jinsia imeoneshwa kama ifuatavyo:
Kwanza, mwanamke ameoneshwa kuwa ni mtu mwepesi/rahisi kujiingiza katika uasharati. Katika hadithi ya Hamnazo mwandishi amemuonesha Mwanahija kuwa ni mwanamke ambaye aliyetakiwa na wanaume kimapenzi lakini alikuwa mgumu kujiingiza katika masuala hayo ila baadae alikubali. Mfano wa hayo unaonekana katika ukurasa wa 43 mwandishi aliposoma “…pale alipojitia ugumu mpaka alipolainika kwa haja na mahitaji. Na alipojisabilia akawa kinyang’anyiro katika ulimwengu muuchu unaouza na kununua kila kitu…”
Vilevile katika jamii jinsia ya kike (wanawake) wanapotakiwa na wanaume kimapenzi, kwanza hukataa lakini baadae hukubali na kujiingiza katika uasharati.
Pia katika hadithi fupi ya Hamnazo, mwanamke ameoneshwa kama ni mtu anaependa starehe na ulevi. Mwandishi amemuonesha Mwanahija kuwa anapenda starehe na ulevi katika uk.13 pale aliposema, “…na bila shaka tafrija ya jana alifuzu, na kikao cha ulevi kilikuwa raha tupu”. Aidha katika jamii baadhi ya wanawake wanajiingiza katika ulevi na kupenda starehe.
Kwa kuongezea mwanamke ameoneshwa katika hadithi hii kuwa hufikia muda hadhi yake aliyokuwanayo wakati wa ujana wake hushuka. Mwanahija ameoneshwa wakati wa ujana wake alikuwa akitumia vitu vya thamani kama vile poda, manukato, nakadhalika lakini baada ya muda kumpita alivikosa vitu vya thamani na akawa na vitu vyenye thamani duni. Ushahidi wa hayo tunaupata katika uk. 43 kwa kusema:
“siku nyengine alikaa yeye mwenyewe akastaajabu kwamba aliwahi kutumia poda na manukato ya thamani namna ile, na sasa akijitazama alivyo, kanzu anazovaa, mafuta ya mkokoriko, wanja wa masizi na poda ya chokaa ya chumba chake. Ilighasi. Iliuma”. Pia katika jamii jinsia ya kike inapokuwa katika ujana inakuwa na mambo ya thamani lakini inapopitwa na ujana inavikosa vitu hivyo.
Vilevile jinsia ya kike, katika hadithi ya Hamnazo imeoneshwa ni watu ambao wana jeuri kwa wenzao. Mwadishi amemuonesha muhusika Mwanahija kuwa ni jeuri kwa wenzake, akiambiwa kitu hamjibu aliyemwambia wala hasalimii wenziwe. Ushahidi wa hayo unaonekana katika uk. 44 mwandishi aliposema: “kama kawaida Mwanahija aliyekuwa na jeuri kwa wenzake, aliubana kimya, akafungua mlango, akampita mwenzake bila hata kumtajia “kwi”. He hata mamaangu hunitukani?...” Aidha katika jamii baadhi ya wanawake wanakuwa wajeuri kwa wenzao wanapoambiwa kitu wananyamaza kimya wala hawawasalimii wenzao.
Kwa upande wa jinsia ya kiume wameoneshwa katika hadithi ya Hamnazo kuwa ni watu hadaa na wasio aminika. Mwandishi amemuonesha muhusika Kitwana kuwa ni mwanamme ambae anataka kumfanyia Mwanahija mambo mabaya. Hali hii imeoneshwa katika ukurasa wa 44 pale Bi Mtumwa alipomwambia Mwanahija, “Basi bibi kaja bwana hapa na mjo wake haukunikalia sawa, alitaka kukuona, nikamwambia hupo. Mimi namuona mwaume yule kanikalia vibaya kweli kweli. Anakitu anataka kukufanya…” Pia baadhi ya wanaume katika jamii wanawahadaa wanawake kwa kuwambia wanawapenda kumbe wanataka kuwafanyia vitu vibaya.
Aidha katika hadithi ya Hamnazo, mwanamke ameoneshwa ni mtu anaesahau maovu anayofanyiwa na mwanamme na kuwa mwenye huruma. Hayo yameoneshwa kupitia muhusika Mwanahija kuwa alikuwa na mpenzi wake Kitwana ambaye waliachana, lakini baada ya Kitwana  kurudi na kumtaka tena Mwanahija, alikubali kurudiana nae. Hayo yameoneshwa katika uk. 44 kwa kusema: “Toka alipokuwa akikoga mpaka alipomaliza, aliwaza juu ya mfululizo wa kibwana nyumbani kwake, baada ya utengano wa muda mrefu. Mwisho Mwanahija aliamua kwa ushujaa, “kufa ndio mwisho wa mja… Kitwana na atende apendalo”…akaupura kwa kiasi chake alitoka bila ya kumuaga Bi Mtumwa”. Vile vile wanawake wengi katika jamii baada ya kufanyiwa maovu na mabwana zao au waume zao wanakuwa ni wepesi wa kusamehe na kurudiana nao.
Kwa kuendelea na hadithi ya Jiarani Mwaminifu nafasi ya jinsia imeoneshwa kama ifuatavyo:
Kwa kuanzia na jinsia ya kiume imeoneshwa kwamba wanaume ndio wasimamizi wakuu wa familia na wanapaswa kuzilinda na kuhakikisha usalama wa familiya zao. Katika hadithi hii Bwana Saidi alikuwa mkali kwa watoto wake na hakuwaruhusu kutoka nje na kubwa zaidi katika nyumba yake hakuruhusu mwanamme yoyote kuingia. Mfano mwandishi anasema katika uk.51 kuwa, “ Bwana Saidi alikuwa baba mkali. Watoto wake wa kike kabisa hakuwaruhusu kutoka nje na ndani ya nyumba yake hakumuachia mwanamume yoyote kuingia”. Aidha katika jamii wanaume ndio wasimamizi wakuu wa familia zao na huzilinda na kuhakikisha usalama wa familia hizo.
Pia hadithi hii imeonesha jinsia ya kike kwamba wanawake ni watu ambao hawaaminiki hata uwaone wana imani nzuri ya dini lakini wanafanya mambo machafu kwa siri ya hali ya juu. Hali hii imejitokeza katika uk. 52 kupitia muhusika Bi Mtumwa ambaye aliaminika kuwa ni mcha Mungu, yaani mtu mwenye imani ya dini na kukesha usiku kwa kufanya ibada. Lakini kumbe usiku ule hakuwa akikesha kwa kufanya ibada isipokuwa alikesha kwa kufanya uovu, yaani alikesha na mwanamme. Mwandishi ameeleza hivi:
“… watoto walipelekana chooni wakati wa kurudi mmoja ghafla alitupa jicho nje. Bibi mmoja alikuwa katandika kizulia uwanjani kakaa na kijana wa kiume. Polepole watoto waliingia chumbani kwao wakazima taa halafu wakanyatia mpaka kwenye dirisha lao lililokuwa limefungwa wakachungulia kwenye virukia. Walipotazama vizuri walimuona Bi Mtumwa. Baada ya kujifurahisha kwa muda walinyemelea wakarudi vitandani mwao”. Aidha katika jamii wapo baadhi ya wanawake ambao wanaonekana ni wachamungu kumbe ni kinyume chake, huwa wanafanya maasi kwa kuwa na wanaume ambao hawajawaoa.
Vilevile katika hadithi ya Jirani Mwaminifu jinsia ya kike imeoneshwa ni watu wanaoishi vizuri na  majirani zao na kuwa tayari kusaidiana pindi mmoja akipatwa na matatizo. Haya yameoneshwa kupitia muhusika Bi Mtumwa alipokubali kwenda kukaa na watoto wa Bwana Saidi siku ile ambayo walifiliwa na iliwabidi waende shamba katika msiba yeye na mkewe. Ushahidi wa haya umeoneshwa katika uk.52 mwandisi aliposema, “usiku ulipoingia Bi Mtumwa alifika. “sasa watoto tukishakunywa chai mwende zenu kupumzika”. Pia katika jamii wako baadhi ya majirani ambao wanaishi vizuri na wanaelewana , vilevile wako tayari kusaidiana pindi mmoja anapofikwa na tatizo.
Kwa upande wa hadithi fupi ya Ulimi wa Da Msimu imeonesha nafasi ya jinsia ya kike na ya kiume kama ifuatavyo:
Kwa kuanzia na jinsia ya kiume, mwandishi ameionesha jinsia ya kiume kuwa ni watu wanaotumia mamlaka yao vibaya kwa kuwatawisha wake zao ndani bila ya kutoka nje wakati wanapoondoka. Hali hii inaonekana kupitia Machano ambaye aliondoka kwenda shamba na kurudi baada ya siku mbili, hivyo alimwambia mkewe ambaye ni Ashura asitoke akiwa yeye hayupo. Mwandishi ameionesha hali hii katika ukurasa wa 79 pale Machano aliopomwambia mkewe, “mimi ninakwenda shamba nitarudi kesho kutwa nikijaaliwa. Lakini sitaki utoke nikiwa sipo”. Aidha katika jamii wapo baadhi ya wanaume wanaotumia mamlaka yao vibaya kwa kuwatawisha wake zao wasitoke nje pindi wakiondoka.
Aidha jinsia ya kike imeoneshwa kuwa ni watu wakarimu. Ukarimu unaonekana kupiti Ashura ambaye alimsisitiza mumewe aende na zawadi shamba, pia alimkirimu chai na uji jirani yake ambaye ni Da Msimu baada ya kwenda nyumbani kwake. Haya yameoneshwa katika ukurasa wa 79 Ashura aliposema:
“Nenda na kizawadi urudi na kipakacha”.
 “… karibu Da Msimu… chai,uji, karibu hiyo”.
“vyote vipo usitie wasiwasi”.
Pia jinsia ya kike katika jamii wanakuwa ni watu wakarimu kwa wageni wao na kuwahimiza waume zao wanapoondoka wachukue zawadi ili wawapelekee wanakokwenda.
Pia katika hadithi ya Ulimi wa Da Msimu imeoneshwa jinsia ya kike ni watu washawishi na wafitinishaji wa ndoa za wenzao na kuwa wasaliti. Hayo yameoneshwa kupitia muhusika Da Msimu ambaye alimshawishi Ashura aende katika beni bila ya ruhusa ya mumewe na kumshawishi alewe. Ashura alifanya kama alivyoambiwa na Da Msimu. Hayo yanaonekana katika ukurasa wa 80-82 kwa kusema:
“kwanza atajuaje kama umekwenda?” Msimu alimwambia Ashura… sura mbilimbili babu we, utamwambia alikuwa mtu mwengine huyo.” Lakini baadae alipata matatizo ya kuumia mguu na kuchunika uso. Baada ya kupatwa na matatizo hayo Da Msimu alimgeuka Ashura na kumwambua atajijua na mumewe. Pale aliposema, “ mtu akiambiwa na yeye hujiambia ati, ukiambiwa twende utakwenda tu, au fanya utafanya tu? Atatambuana mwenyewe na mumewe”. Vile vile katika jamii wanawake wanaonekana kuwa ni washawishi , wafitinishaji wa ndoa za wenzao na huwasaliti baada ya wenzao kupatwa na matatizo.
Vilevile hadithi hii imeonesha jinsia ya kike ni yenye kupinga amri za waume zao. Hali hii tumeiona kupitia Ashura ambaye aliamua kwenda katika beni ingawa aliambiwa asitoke nje na mumewe wakati akiondoka. Mwandishi ameionesha hali hiyo katika ukurasa wa 80 kwa kusema:
“Ashura alikuwa katikati kazongwa haonekani, kachukuliwa kabisa na ngoma hasikii haoni…”
Pia katika jamii wapo wanawake ambao wanapinga amri za waume zao wanapoambiwa wasitoke nje ikiwa waume zao hawapo, lakini huwa wanatoka nje na kwenda wanakopenda.
Kwa kumalizia na hadithi fupi ya Mtu na haki yake nafasi ya jinsia imeoneshwa hivi:
Kwanza jinsia ya kiume imeoneshwa kuwa ni wafanyabiashara. Katika hadithi fupi ya Mtu na haki yake imeoneshwa jinsia ya kiume kuwa ni wafanyabiashara kupitia kijana aliyekuwa anauza kofia ya viua vya lasi. Mwandishi amemuonesha kijana huyo katika ukurasa wa 25 aliposema:
“Khamis alipomwona kijana mmoja anazabuni kofia ya viua vya lasi njiani na yeye alisimama.
“Je, biashara hiyo?”aliuliza.
“Ndio”, alijibu mwenye kofia…”
Aidha katika jamii jinsia ya kiume inajishughulisha zaidi katika kufanya biashara ya kurandisha vitu (bidhaa) mitaani kuliko jinsia ya kike.
Kwa kuongezea, jinsia ya kiume imeoneshwa kwamba ni watu matapeli. Katika hadithi ya Mtu na haki yake wanaume wameoneshwa kuwa ni matapeli. Kupitia Khamis ambaye alitaka kumtapeli muuza kofia kwa kuichukuwa kofia yake na hakuwa na lengo la kumlipa. Khamis ameoneshwa katika uk. 25-26 utapeli aliokuwa anataka kumfanyia muuza kofia kwa kusema: “Khamis hajawa na mpango maalumu: alibaki kutegemea bahati tu. Alikuwa na tamaa kwamba labda anaweza kufanya njia hata atokee kwa mlango wa nyuma wa Chuo na kupotelea mbali”. Pia katika jamii jinsia ya kiume kwa kiasi kikubwa ndio wanaoongoza kwa kutapeli wenzao katika biashara.
Vilevile, jinsia ya kike imeoneshwa kuwa ni waalimu wa Chuoni (Madrasa). Katika hadithi hii mwanamke ameoneshwa ni mwalimu wa Chuo cha Qur-ani katika ukurasa wa 26 ambapo mwandishi amesema:
“Bi Mwalimu nina mwanangu nataka kumtia Chuoni, “ Khamis alimwambia Bi Mwalimu baada ya kumuamkia kwa adabu”. Aidha wapo wanawake katika jamii ambao ni waalimu wanaosomesha katika vyuo vya Qur-ani (Madrasa).
Pia katika hadithi ya Mtu na haki yake jinsia ya kiume imeoneshwa ni wafanya kazi wa serikali katika Wizara ya Ulinzi (Askari). Wanaume katika hadithi hii wameoneshwa kuwa ni askari ambapo miongoni mwa kazi zao ni kuwakamata wanaodhulumu wenzao. Kwa hivyo Khamis baada ya kuona askari alifadhaika kutokana na utapeli ambao alikuwa anataka kuufanya. Haya yameoneshwa katika ukurasa wa 26 mwandishi aliposema:
“kutupa jicho nje aliona askari wawili wanasogelea upande wa Chuoni: ubabaifu na hofu ulichanganyika kumfanya mwehu ghafla”. Vilevile katika jamii wapo wanaume wanaofanya kazi ya uaskari: Pia kuna baadhi ya watu wanapowaona askari ikiwa wamefanya kosa wanakuwa na ubabaifu na kuogopa kukamatwa.
Kutokana na maelezo ya hadithi fupifupi nne nilizozitumia ambazo ni hadithi ya Hamnazo, Jirani Mwaminifu, Ulimi wa Da Msimu na hadithi ya Mtu na haki yake, hivyo ndivyo jinsi nafasi ya jinsia ilivyooneshwa katika hadithi fupifupi za Kiswahili.


MAREJEO
M, M. Mulokozi. (1996). Fasihi ya Kiswahili. Tanzania: Chuo Kikuu Huria cha Tanzania.
Mohammed, S. A & Ali, A. M. (1981). Hapa na Pale. Zanzibar: Taasisi ya Kiswahili na Lugha za
                                                                Kigeni/Wizara ya Elimu.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni