Jumanne, 5 Julai 2016



BAHARI IMECHAFUKA

Bahari imechafuka,  samaki wakimbizana
Na hali ikachafuka ,  kuona wakipishana
Buhuri ikasikika ,  kama kwamba ni mchana
Wanaruka kwa hasira , samaki hawa jamani.

Wakubwa waliwacheka , wadogo zao kwa sana
Kuona wadhalilika , kukosa yao hiyana
Wengi wao kukereka , kuonewa na mabwana
Wanaruka kwa hasira , samaki hawa jamani

Furaha yao kufika , katika kila kona
Ingawa si ya mipaka, lakini yatakikana
Itakuwa  patashika , kelele kila namna
Wanaruka kwa hasira , samaki hawa jamani

Maji haya yazunguka , kwa wimbi lisonekana
Samaki mekushanyika , wamejazajazana
Mawimbi yanasikika , watu kazi kunong´ona
Wanaruka kwa hasira , samaki hawa jamani

Haya twende kwa haraka , samaki wakimbizana
Ni yetu hiyo sadaka , wakubwa watakikana
Muafaka kuweka ,  tusije hitalifiana
Wanaruka kwa hasira , samaki hawa jamani

Ndani ya hili shitaka , musije mukatuona
Ndimi zetu ni mashaka , kwa tunayoambizana
Ndo mimi na huyu kaka , tulivyokwisha nong'ona
Wanaruka kwa hasira ,  samaki hawa jamani

Tangu kale hadi leo , hatujaona lamana
Tena kwa ukali wao ,eti wanafokeana
Toeni zote komeo , tunataka kupambana
Wanaruka kwa hasira , samaki hawa jamani

Ajira sasa haziko , wapi zapatikana
Tunataka mabadiliko , hebu tizameni sana
Kutwa ni mahangaiko , usiku tunakabana
Wanaruka kwa hasira , samaki hawa jamani

Kama nyinyi hamuwezi , sisi tunatakikana
Kudai yetu agizi , kwa wanaotubana
Tunataka mageuzi , wazee pia vijana
Wanaruka kwa hasira , samaki hawa jamani

Vijana tuunganeni , kudai yetu hiyana
Ili tuishi duniani , bila ya kuoneyana
Wakubwa wamapangoni , wameridhika na ubwana
Wanaruka kwa hasira , samaki hawa jamani.


SAADA MABROUK JUMA- CHAWAKAMA SUZA

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni