NAMNA
USHAIRI UNNAVYOFANANA NA KUTAFAUTIANA NA NGONJERA
NA:SALEH ZAHRAN----CHAWAKAMA-SUZA
Katika makala
hii tutaangalia katika sehemu kuu nne. Kwanza tutaeleza fasili ya Ushairi na Ngonjera
kwa mujibu wa wataalamu mbalimbali. Pia tutaeleza tafauti za ngonjera na
ushairi. Vile vile tutaeleza mfanano wao
na mwisho tutamalizia na hitimisho.
Kwa kuanzia na
fasili mbalimbali:
Kwa mujibu
wa Masebo ( 2001) anasema ushairi ni
sanaa inayopambanuliwa kwa mpangilio
maalum wa maneno fasaha na yenye muwala, kwa lugha ya mkato, picha au sitiari au ishara, katika usemi, maandishi au
mahadhi ya wimbo ili kueleza tukio, wazo au hisi fulani kuhusu maisha au
mazingira ya binaadamu, kwa njia inayogusa moyo.
Pia ushairi ni kazi za fasihi zinazojumuisha
matumizi ya mapigo ya kimuziki. (Kaduguda na wenzake 2009).
Kiujumla
tunasema kuwa ushairi ni tanzu ya fasihi ambayo hutumia lugha nzito, ya mkato,
matumizi ya lahaja, fasaha ili kufikisha ujumbe uliokusudiwa ambapo kwa upande
wa ngonjera ni kai ya fasihi ambayo hutumiya lugha tafauti na ushairi.
Ngonjera kwa
mujibu wa BAKIZA (2010) ni ushairi unaotambwa kwa njia ya maigizo ya
majibizano.
Vilevile
ngonjera ni mashairi ya kujibizana baina ya watu wawili au zaidi. (Mvungi,
2010).Kwa ujumla ushairi na ngonjera unaonekana kutafautiana sana na hii ni
kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo:-
Ushairi ni kati ya tanzu kuu nne za fasihi simulizi
ambazo ni ushairi, semi, maigizo na hadithi
ilihali ngonjera ni kati ya kipera cha ushairi chenyewe ambacho ni
mashairi, tenzi, nyimbo, maghani na ngonjera.
Ushairi unakuwa
na wazo moja linaloelezea juu ya jambo fulani wakati ngonjera huwa ni wazo moja
lenye majibizano bila ya kuwepo majibizano haitokuwa ngonjera.
Halikadhalika
ushairi una vipera vingi kama vile ngonjera, maghani, tenzi, tumbuizo lakini
ngonjera haina vipera ndani yake chenyewe ni kipera cha ushairi.
Pamoja na hayo ushairi
huweza kughaniwa na muhusika mmoja wakati ngonjera hutambwa au kuigizwa kuanzia
wahusika wawili na kuendelea.
Vilevile ushairi
hufuata kanuni zote za kimapokeo, kimamboleo pamoja na kimajaribio lakini
ngonjera hufuata kanuni ya kimapokeo tu. Mfano beti, vina, mizani, urari,
kibwagizo, muwala nk huwa ni sawa kama vile zilivyo kwenye mashairi ya
kimapokeo tu.
Pia majibu au suluhisho la ushairi hutolewa na mhakiki
anayeisoma kazi hiyo ya ushairi lakini ngonjera suluhisho lake hutolewa na watambaji
wenyewe au mtunzi aliyetunga kazi hiyo mwisho wa ngonjera yenyewe.
Ushairi hutumia
lugha ya mafumbo na lugha ya mkato lakini ngonjera hutumia lugha nyepesi na
sanifu ambayo msikilizaji au mtazamaji huweza kufahamu kwa urahisi zaidi.
Mfano wa shairi
ambalo limetumia lugha ya mkato. Lugha hii imeweza kutowa ujumbe uliokusudiwa.
Katika kitabu cha Kimbunga uk: 12.
RUSHWA
Rushwa kajenga kambi, na kuondoka hataki
Afanya kila vitimbi, mkaidi hashindiki
Tumzushieni wimbi, isiwe kutuhiliki
Tumchimbie handaki, rushwa tukamzikeni.
Mfano wa
ngonjera ambayo haiwezi kutumia lugha ya mkato kutokana na muundo wake. Katika
kitabu cha Kiswahili kwa Shule za Sekondari Kidato cha 2 uk: 111
CHUMA:
Ndugu
tega sikio, maoni
kutekeleza,
Mwisho nipe
itikio, kwayo niliyoeleza
Pasiwepo
singizio, au yangu kuyabeza,
Rushwa ndani ya
haki, haifai kutumia.
SHOMVI:
Nakuona wajivunga, hunalo la maana,
Na kamwe hayana
mwanga, nieleweni bayana,
Kaa njaa ukiganga, ukidhani rushwa lana,
Bila kupokea rushwa, tumbo haliwezi shiba.
Ushairi
hauzingatii mambo ya uigizaji katika jukwaa lakini ngonjera inazingatia mambo
muhimu ya uigizaji katika jukwaa kama vile maleba, matumizi ya vifaa vya
uigizaji pamoja na vitendo vya wahusika jukwaani.
Ushairi unaweza
kuwa na idadi nyingi au idadi chache ya
beti ( beti moja) na kuweza kutosheleza kinachozungumzwa lakini ngonjera
haiwezi kuwa na idadi chache (beti moja)
na kuweza kujitosheleza. Mfano shairi la Rushwa uk: 12 katika kitabu cha
Kimbunga lina beti moja yenye kujitosheleza na shairi Macho uk: 27
katika kitabu cha Raha Karaha lakini pia shairi la Rushwa katika kitabu cha
Kimbunga.
Mbali na tafauti
hizo zilizojitokeza kati ya usahiri na ngonjera pia kuna mlingano wake nazo ni
-:
Ushairi na
ngonjera ni tanzu za Fasihi Simulizi ingawa ngonjera haijitegemei kama ulivyo
ushairi.
FASIHI SIMULIZI
|
|||
HADITHI
|
USHAIRI
|
SEMI
|
MAIGIZO
|
|
Ngonjera,
maghani mashairi, tenzi, nyimbo
|
|
|
Pia zote kwa
pamoja hutumia beti na urari wa mizani na vina. Mfano wa ubeti wa shairi wenye urari wa vina na mizani.
Ja/ma/ni/ ni/me/i/cho/ka, a/dha/ hi/i/ si/i/ta/ki
Mnyonge nadhalilika, nchini sihitajiki
Hakuna kinacholika, nilacho hakisemeki
Kwangu tabu na
mashaka, kama uji na mgonjwa.
Mfano wa ubeti
wa ngonjera wenye urari wa vina na mizani.
Ado: Wa/li/mwe/ngu/ na/u/l/iza, ma/ji/bu/ m/ni/pa/t/ie,
Kichwani naona kiza, utando mnifutie,
Acheni kuniburuza, maelezo tafutie,
Ajira kwao watoto, tija gani mnapata?
Vilevile ushairi
na ngonjera hughaniwa katika mahadhi tafauti itategemea na uamuzi wa wanaoghani hiyo ngonjera au
ushairi.
Halikadhalika
zote kwa pamoja hutowa hisi na tafakuri katika ulimwengu. Mfano hisia na
msisimko juu ya ugonjwa wa Kipindupindu,
UKIMWI, Mauaji ya Albino Ajira kwa watoto nk.
Ngonjera na
ushairi huwasilishwa jukwaani, katika kumbi mbalimbali, katika sherehe mbalimbali na
kwenye vyombo vya habari.
Aidha zote
hutumia ubunifu wa lugha ambao huleta mdundo na msisimko wakati wa kuimbwa,
kughaniwa au kuigizwa. Mdundo hupatika katika urari wa vina vilivyotumiwa
katika shairi au ngonjera.
Ngonjera na
ushairi hutumia mtindo wa masimulizi katika kuonyesha wakati na mandhari iliyotumika.
Mfano wa shairi
ambalo limetumia mtindo wa masimulizi ni shairi Kibwangai uk : 9 katika kitabu
cha Kimbunga.
Kuna hadithi ya kale, kwa babu nimepokeya
Kwa
manyani zama zile, mkasa ulotokeya
Nilikuwa mwanakele, hayo nikazingatia
Leo nawadokezeya, kwa nilivyoyafahamu.
Mfano wa
ngonjera ambayo imetumia masimulizi ni ngonjera ya Ujamaa Vijijini uk : 107
katika kitabu cha Kiswahili kwa shule za Sekondari kidato cha pili.
Msimulizi
“Kijana aliingia, ndani kutoka shuleni,
Kakuta waongea, wazaziwe sebuleni,
Hima aliamkia, na akaketi kitini,
Mara mama kwa huzuni, sauti ikamtoka”
Kutokana na
maelezo hayo ngonjera na ushairi zinatafautiana na kulingana kwa kuziweka
pamoja katika nyanja za ushairi. Kwahiyo
tunaona ni jinsi gani zilivyotafautiana katika tanzu na vipera, namna ya uwasilishaji wake, wahusika, katika
kanuni zake, utowaji wa suluhisho, matumizi ya lugha, idadi ya beti pamoja na
mambo ya kuzingatia wakati wa kuigiza. Halikadhalika shairi na ngonjera
hufanana katika utanzu wa fasihi simulizi, urari wa beti wenye kuzingatia
mizani na vina, utoshelevu wa beti, hutumika katika mukhtadha maalum, hutumia
ubunifu wa lugha wenye kutowa msisimko na mdundo ndani yake, mtindo wa
masimulizi pamoja na kutowa hisi na tafakuri.
MAREJEO
BAKIZA (2010). Kamusi la Kiswahili Fasaha. Oxford University Press. Dar- es- salaam.
Masebo, J. A na Bukagile, G, R. (2007). KISWAHILI;
KWA SHULE ZA SEKONDARI. Kidato cha Pili. Nyambari Nyangwine
Publishers: Dar Es Salaam.
Kaduguda, R. Na wenzake ( 2009) Kiswahili
Shule za Sekondari, Kidato cha Kwanza. Oxford University Press: Tanzania.
Mvungi, Th. A. (1982). Raha Karaha. CONTINENTAL
PUBLISHER LIMITED: Dar es salaam.
Haji, G. H. ( 1998). Kimbunga. Dar es salaam University Press. Dar es
salaam.
Mvungi, Th, A ( 2010 ). Kiswahili Kidato cha 1 na 2. Ben
and company Ltd. Dar- es -salaam.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni